Home Traders

Home Traders

Tembelea TK FM Redio 88.5 Tanga

Tuesday, 26 August 2014

Saa 24 za hatari kwa Okwi, Mosoti

Zanzibar. Saa 24 zimebaki kabla ya mshambuliaji, Emmanuel Okwi wa Yanga na beki Donald Mosoti wa Simba kutangazwa kuwa si wachezaji wa klabu hizo.
Viongozi wa Simba na Yanga wanajua kuwa kesho ni siku ya mwisho ya kufanya usajili hivyo wanatakiwa kufanya uamuzi sahihi ni wachezaji gani wanataka kuendelea kuwa nao kati ya Mosoti au Butoyi Hussen kwa Simba na Okwi au Hamis Kiiza kwa upande wa Yanga.
Yanga ina wachezaji sita wa kigeni kama ilivyo kwa Simba, lakini kuachwa kwa Okwi na Mosoti kutategemea nguvu ya hoja kati ya makocha na viongozi wa timu hizo kubwa nchini.
Mbrazili Marcio Maximo ameshaweka wazi kuwa anawajua wachezaji watano wa kutoka nje katika kikosini chake bila ya kumjumuisha Okwi.
Maximo alisema: “Ninao wachezaji watano tayari wa kutoka nje ya nchi kwenye timu yangu, hao ndiyo nitakaofanya nao kazi msimu huu.
“Huyo Okwi sijamuona na hadi leo hajaripoti kwenye timu yangu nifanyeje? Nitafanya kazi na hao tu.” Maximo ana wachezaji wa kigeni, Kiiza (Uganda), Wanyarwanda Haruna Niyonzima na Mbuyu Twite pamoja na Wabrazili Andrey Coutinho na Santos Santana ‘Jaja’.
Lakini, Yanga ina mkataba na Okwi hivyo kufanya kuwa na wachezaji sita, idadi ambayo hadi kesho siku ya kufunga dirisha la usajili, itatakiwa kupunguza mmoja.
Wakati hali ikiwa hivyo Jangwani, viongozi wa watani wao Simba, juzi walikutana Zanzibar  ili kumaliza suala la usajili wa beki wao mpya, Mrundi Butoyi  na kumtema Mosoti.
Viongozi hao waliokutana ni Makamu wa Rais, Geofrey Nyange ‘Kaburu’, Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili, Kassim Dewji, Mjumbe na Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Ufundi, Collins Frisch, Mwenyekiti wa Kamati ya Mashindano, Mohammed Nassoro na Makamu wake, Idd Kajuna pamoja na wajumbe, Adam Mgoyi, Mohamed Omary na Hussein Simba.
Dewji alisema wameangalia viwango vya wachezaji wao na kuridhika kuwa Butoyi amecheza kwa kiwango cha juu zaidi.
Kuhusu hatima yake alisema itajulikana ndani ya siku mbili baada ya kukaa na kocha ili kuamua nani abaki kati ya Mosoti na Butoyi, ingawa inasemekana pendekezo lao ni kumsajili Butoyi.
“Dirisha la usajili linafungwa Jumatano ni lazima tufanye uamuzi kati ya siku hizi mbili, timu yetu ipo vizuri sasa hivi na upungufu tulionao tutazungumza na kocha ili arekebishe mapema.
“Butoyi tumemwona, ni mchezaji mzuri na kikubwa hapa ilikuwa ni kujiridhisha tu ila hatuwezi kufanya lolote mpaka tukutane na kocha ambaye pia amemuona kwenye mazoezi,” alisema Dewji.
Lakini habari za ndani zinasema kikao hicho kilimalizika saa nane usiku bila kufikia uamuzi.
“Walitaka kufanya uamuzi wa kumpa mkataba Butoyi, lakini kocha amewaambia wasubiri kwanza atawapa jibu kabla ya usajili kufungwa.
“Wengi wanataka Butoyi asajili kwani kigezo wanachotumia ni kwamba Mosoti umri umekwenda, kiwango chake kimeshuka na alionyesha kutaka kuondoka hivyo wanataka wamwachie awe huru.”
Kocha wa Simba, Patrick Phiri alisema: “Ni lazima nifanye uamuzi sahihi, leo (jana) jioni nitakuwa na jibu kuhusu nani kati ya hao atabaki, ila Butoyi na Mosoti wote ni wazuri.”
Chanzo Mwananchi

No comments:

Post a Comment