Home Traders

Home Traders

Tembelea TK FM Redio 88.5 Tanga

Monday, 25 August 2014

UDA wamiliki Daladala wapongezwa

UONGOZI wa Shirika la Usafiri Dar es Salaam (UDA), pamoja na wamiliki wa daladala mkoa wa Dar es Salaam, wamesaini mkataba wa makubaliano ya kushirikiana kwa lengo la kushinda zabuni ya kuendesha mradi wa mabasi yaendayo haraka (DART) jijini Dares Salaam.
Utiaji saini huo, ulifanyika jijini DaresSalaam mwishoni mwa wiki kwenye ukumbi wa mikutano wa kimataifa wa Mwalimu Julius Nyerere na kushuhudiwa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), Hawa Ghasia na Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Said Meck Sadiki.
Akizungumza katika hafla hiyo, Waziri Ghasia alisema uamuzi uliyochukuliwa na UDA na wamiliki wa daladala ni mfano wa kuigwa nchini.
Alisema kuungana kwao pamoja, kutawajengea mazingira bora ya kuaminika zaidi, ambayo yatatoa ushindani madhubuti dhidi ya kampuni za nje zitakazojitokeza kuomba kuendesha mradi wa DART.
Pia, alimpongeza Mwenyekiti wa Saimon Group, Robert Kisena na viongozi wa vyama vya wamiliki wa daladala Mkoa wa Dar es Salaam kwa uamuzi huo wenye tija kwa taifa, kwani utaongeza ajira zaidi na kupunguza umasikini.
Uamuzi huo, ulifikiwa baada ya mkutano wa mafanikio uliyofanyika Ijumaa iliyopita kwenye ukumbi wa Karimjee ulioandaliwa na kamati teule ya wamiliki wa daladala jijini Dar es Salaam na kuwakutanisha wamiliki wote.
Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa Said Meck Sadiki, alisema kuunganisha nguvu kwa wadau hao kutatoa fursa kwa serikali kuwaunga mkono katika jitihada zake za kuboresha hali ya usafiri Dar es Salaam.

Naye Mwenyekiti Mtendaji wa Saimon Group inayomiliki UDA, Robert Kisena, alisema watafungua milango kwa wamiliki hao kununua hisa zitakazowezesha mtu yeyote kuwa mkurugenzi.
“Pia tunatoa wito kwa wananchi mbalimbali kujitokeza kununua hisa kwa wingi zaidi ili kuhakikisha tunaboresha huduma ya usafiri katika jiji hili,” alisema Kisena.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Darcoboa, Sabri Mabrouk, alisema kutokana na UDA kuwa kampuni yenye uwezo, kuna haja ya kuunganisha nguvu kwa pamoja ili kuhakikisha kwamba zabuni itakapotangazwa hakuna kampuni kutoka nje itakayoshinda.

No comments:

Post a Comment